Wednesday, January 25, 2017

WAFANYABIASHARA MAILIMOJA WAHUKUMIWA KIFUNGO CHA NJE.

Na John Gagarini, Kibaha
WAFANYABIASHARA 62 wa lililokuwa soko la Maili Moja wilayani Kibaha mkoani Pwani waliofanya mkusanyiko usio halali na kutaka kumwona Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Seleman Jaffo wamehukumiwa kifungo cha nje cha miezi sita.
Hukumu hiyo ilitolewa kwenye mahakama ya hakimu mkazi wa mahakama ya wilaya ya Kibaha Aziza Mbadjo chini ya mwendesha mashtaka mwanasheria wa serikali Auleria Makundi na mkaguzi wa Polisi Rashid Chamwi.
Mahakama ilielezwa kuwa wafanyabiashara hao bila ya kibali walifanya mkusanyiko huo huku wakiwa na mabango yenye jumbe mbalimbali na kutaka kumwona Waziri Jaffo.
Na walifanya mkusanyiko huo wakitaka kutoa malalamiko yao juu zoezi zima la uhamishwaji wao kutoka soko la Maili Moja ambalo limebomolewa hivi karibuni kwenda soko jipya la Mnarani au Sagulasagula maarufu kama Loliondo.
Ikaelezwa kuwa washtakiwa kwa pamoja walitenda kosa hilo Januari 6 mwaka huu majira ya saa 4 asubuhi eneo la Shirika la Elimu Kibaha (KEC) Tumbi walifanya mkusanyiko bila ya kibali toka Polisi wilaya.
Pia walikuwa na mabango hayo jambo ambalo ni kinyume cha sheria jambo ambalo lilionyesha kuleta usumbufu kutokana na kukosa uhalali wa kufanya hivyo.
Baada ya kusomewa shitaka hilo ambalo ni kinyume cha sheria namba 74 (1-2) na 75 kifungu kidogo cha kanuni ya adhabu kilichofanyiwa mapitio mwaka 2002 walikiri kutenda kosa hilo na walijitetea kwa kusema kuwa walifanya kosa hilo bila ya kujua na wanamajukumu mengi ya kifamilia hivyo kuiomba mahakama iwapunguzie adhabu.
Kutokana na utetezi huo hakimu Mbadjo alisema kuwa kutojua sheria siyo sababu ya kuvunja sheria hivyo mahakama imewakuta na hatia hivyo wanahukumiwa kifungo cha nje ambapo wataitumikia jamii na hawapaswi kufanya kosa katika muda huo.
Mwisho.  


Monday, January 23, 2017

johngagariniblog: BOMOA YATIKISA MAILI MOJA KIBAHA

johngagariniblog: BOMOA YATIKISA MAILI MOJA KIBAHA: Na John Gagarini, Kibaha ZOEZI la kubomoa soko la Maili Moja wilayani Kibaha pamoja na nyumba za biashara na za makazi amba...

BOMOA YATIKISA MAILI MOJA KIBAHA





Na John Gagarini, Kibaha
ZOEZI la kubomoa soko la Maili Moja wilayani Kibaha pamoja na nyumba za biashara na za makazi ambavyo vilijengwa kwenye hifadhi ya barabara limefanyika na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoa wa Pwani chini ya ulinzi mkali wa polisi.
Zoezi hilo ambalo lilianza jana majira ya asubuhi limefanyika baada ya kushindikana kufanyika kwa muda mrefu ambapo mara ya mwisho wameliki wa maeneo hayo walipewa barua na TANROADS miezi sita iliyopita.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake meneja wa wakala hao mkoa wa Pwani Injinia Yudas Msangi alisema kuwa lengo kuu la kubomoa ni kuhakikisha kuwa eneo hilo la hifadhi ya barabara inakuwa wazi.
Msangi alisema kuwa zoezi hilo limefanikiwa kutokana na kuwajulisha mapema wahusika kuwa wabomoe wenyewe kabla ya siku ya kubomoa kufanyika jana Januari 23.
“Tunashukuru kwani hakuna mtu anayelalamika kwa sababu tuliwapa taarifa mapema na wengi wametii kwa kuvunja wao wenyewe na kutoa vitu vyote vya thamani licha ya wachache ambao walishindwa kubomoa wao wenyewe,” alisema Msangi.
Alisema kuwa zoezi hilo kwa Maili Moja ndiyo limehitimisha ubomoaji kwa watu waliojenga kwenye hifadhi ya barabara katika mkoa huo ambapo mwaka jana walibomoa maeneo mengine ya wilaya zote za mkoa huo.
“Baada ya zoezi la kubomoa wananchi hawpaswi kujenga tena kwenye eneo hilo la hifadhi ya barabara ambalo lina matumizi mbalimbali kwa ajili ya magari na shughuli nyingine zinazohusu barabara,” alisema Msangi
Aidha alisema kuwa jana walivunja eneo la umbali wa mita 60 kutoka barabara kuu ya Morogoro ambazo ziko ndani ya hifadhi ya barabara ambayo ilitengwa kwa ajili ya matumizi mengine.
Naye mkaguzi wa barabara Injinia Livingstone Urio alisema kuwa zoezi hilo ni mwendelezo wa usafishaji wa maeneo ambayo ni hifadhi ya barabara ambapo pia ni usalama kwa wananchi kwani ni hatari kujenga au kufanya biashara karibu na barabara.
Urio alisema kuwa eneo hilo lilitengwa kisheria na watu hawakutakiwa kujenga makazi au vibanda vya biashara na wananchi wengi wao wanajua mmiliki wa eneo hilo.
Kwa upande wake mfanyabiashara wa soko la Maili Moja Ally Gonzi alisema kuwa wao wamepokea zoezi hilo kama lilivyo kwani tayari wlaikuwa na taarifa juu ya matumizi ya eneo hilo.
Gonzi alisema kuwa kwa kuwa wametengewa eneo la kufanyia biashara hivyo wataenda huko kwa ajili ya kuendelea na biashara zao licha ya kuwa maandalizi ya soko jipya wamechelewa.

Mwisho.

Friday, January 13, 2017

MATUKIO YA UHALIFU YALIYOTIKISA PWANI 2016


Kamanda wa Polisi mkoa wa Pwani Bonaventura Mushongi akiwaonyesha waandishi wa habari hawapo pichani silaha aina ya SMG no 01304 ikiwa na risasi 30 ya Askari Jackson Shirima  wa Saadani National Park ambaye aliporwa na mtuhumiwa Swalehe Mangupili na kufichwa kichakani huko Kijiji cha Gama wilaya ya Bagamoyo

Na John Gagarini, Kibaha

JUMLA ya makosa makubwa ya uhalifu 4,208 yameripotiwa kwenye vituo vya polisi mkoani Pwani kwa mwaka 2016 ambapo kumekuwa na ongezeko la makosa 419 ikilinganishwa na mwaka 2015 ambao ulikuwa na makosa 3,784.
Aidha makosa madogo 16,332 yaliripotiwa katika kipindi hicho cha mwaka 2016 ambapo kuna ongezeko la makosa 2,396 ikilinganishwa na mwaka 2015 ambapo kulikuwa na makosa 13,936.
Hayo yalisemwa mjini Kibaha na kamanda wa polisi mkoani Pwani Bonaventura Mushongi wakati akitoa taarifa ya mwaka mmoja uliopita na kusema kuwa watu waliohusika na matukio hayo walifikishwa mahakamani.
Mushongi alisema kuwa ongezeko la makosa hayo kumetokana na misako iliyofanywa, doria na oparesheni kwenye maeneo mbalimbali sambamba na ushirikishwaji wa jamii kwenye kufichua uhalifu.
“Tunawashukuru wananachi kwa kuendelea kutupa taarifa mbalimbali ambazo zimesaidia kukabiliana na uhalifu na tunaomba ubia uendelee kwani uwiano wa askari na raia bado hautoshi kwani askari mmoja anahudumia raia zaidi 1,000 hivyo ulinzi shirikishi ni muhimu,” alisema Mushongi.
Alisema kuwa katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita walifikisha mahakamani makosa 1,439 na makosa 159 watuhumiwa walikutwa na hatia na kuhukumiwa kifungo wakati makosa 29 watuhumiwa walishindwa kutiwa hatiani na kuachiwa huru  na makosa mengine kesi bado zinaendelea kwenye mahakama mbalimbali.
“Tumejiwekea mikakati mbalimbali ya kukabiliana na uhalifu kwa kuimarisha vikosi mbalimbali vilivyopo ndani ya mkoa, kuzuia na kutanzua matukio hayo kabla hayajatokea au baada ya kutokea, kuimarisha doria za miguu katika maeneo tete kila wilaya kwa ushirikiano na wananchi,” alisema Mushongi.
Aidha alisema kuwa wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni upungufu wa vitendea kazi ikiwa ni pamoja na uchache wa magari,Jografia ya mkoa kwwenye mipango miji ni ngumu katika kumpata mhalifu kwa haraka pindi uhalifu unapotokea.
“Mwaingiliano na mkoa wa Dar es Salaam unafanya wahalifu kuweza kuingia kirahisi na kufanya makosa,kutokuwa na mpango bora wa matumizi ya ardhi hivyo kusababisha migogoro ya ardhi katika jamii, uwepo wa ukanda wa mkubwa katika bahari unaosababisha kuwepo kwa bandari bubu nyingi za kupitisha wahamiaji haramu na biashara za magendo,” alisema Mushongi.
Alibainisha kuwa mwaka uliopita kulikuwa na matukio makubwa ambayo yaliyovuta hisia za watu ikiwa ni pamoja na kupatikana maiti saba wilaya ya Bagamoyo na mauaji ya viongozi wa serikali za vijiji kwa wilaya za Mkuranga, Rufiji na Kibiti ambapo katika matukio hayo watu 11 walikamatwa  na kufikishwa mahakamani.
Mwisho.