Friday, June 7, 2013

SUMATRA KUDHIBITI MADEREVA PWANI

Na John Gagarini, Kibaha
MAMLAKA ya Udhibiti wa usafiri Majini na Nchini Kavu (SUMATRA) imefungua ofisi yake mkoani Pwani na kuwataka wananchi kutoa taarifa za mabasi yanayokatisha ruti na kutotoa tiketi kwa abiria.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake ofisa mwandamizi wa SUMATRA wa mkoa Iroga Nashoni alisema kuwa abiria wanapaswa kukitumia chombo hicho ili kuondoa kero kwa wasafiri.
Iroga alisema kuwa ofisi hiyo imefunguliwa mwezi uliopita kwa lengo la kusogeza huduma kwa wateja wao ambapo inaendelea kujitanua kwenye mikoa, mingine ikiwa ni Singida, Iringa, Musoma na Rukwa.
Alisema kuwa changamoto kubwa waliyoiona ni mabasi mengi ya abiria kushindwa kumalizia safari zao Kukatisha Ruti) na kutotoa tiketi kwa abiria jambo ambalo ni kinyume cha sheria ambapo watawapiga faini hata ikibidi kuwafungia leseni madereva watukutu.
“Changamoto hiyo inakuwa kubwa kutokana na abiria wengi kutokuwa na elimu ya kujua haki zao za msingi wanapokuwa wanasafiri hivyo kuwapa mwanya madereva kufanya watakavyo,” alisema Iroga.
Aliongeza kuwa wataendelea kutoa elimu kwa pande zote ikiwa ni pamoja na abiria, madereva na wamiliki wa mabasi hayo ili waweze kufuata sheria bila ya kushurutishwa.
“Jana tulifanya operesheni kukamata magari yenye makosa mbalimbali ambapo magari manne yamekutwa na makosa na kupigwa faini kutegemea na makosa,” alisema Iroga.
Alibainisha kuwa wataendelea kufanya operesheni za kushtukiza za mara kwa mara ili kukabiliana na madereva wengi kukiuka sheria za barabarani na kuwataka wananchi kutoa taarifa na si kulalamika bali wachukue hatua.
Mwisho.

MBUNGE AMWAGA VIFAA TIMU YA UMISSETA

Na John Gagarini, Kibaha
MBUNGE wa Jimbo la Kibaha mkoani Pwani Silvestry Koka ametoa seti za
jezi kwa timu za mpira wa pete na soka za mkoa huo zinazojiandaa na
mashindano ya Umoja wa Michezo na Sanaa kwa Shule za Sekondari
Tanzania (UMISSETA) Kanda ya Mashariki inayotarajiwa kutimua vumbi
hivi karibuni mjini Kibaha.
Jezi hizo zimekabidhiwa kwa timu hiyo na mke wa mbunge huyo Selina
Koka kwenye kambi ya timu hiyo iliyopo kwenye shule ya Filbert Bayi
iliyopo wilayani Kibaha.
Mbali ya jezi hizo pia timu ya mkoa iliahidiwa kupatiwa mipira ya
michezo hiyo, mchele, kilogramu 100, mafuta ya kupikia, maji na sukari
pamoja na kumkabidhi mwalimu wa timu hiyo Loyd Mgombele kiasi cha
shilingi 100,000 kwa ajili ya shughuli za kuratibu timu hiyo.
Akiwakabidhi manahodha wa timu ya mpira wa pete na mpira wa miguu Koka
alisema kuwa lengo la kutoa vitu hivyo ni kuhamasisha timu hiyo ili
iweze kufanya vizuri kwenye michezo yake dhidi ya mkoa wa Morogoro ili
kuunda timu ya Kanda.
Koka alisema kuwa mkoa wa Pwani ni wenyeji wa mashindano hayo
wanapaswa kuwa na maandalizi mazuri ili kuweza kuwakilisha vema mkoa
na baadaye Taifa ambapo michuano hiyo itafanyika kwenye viwanja vya
Shirika la Elimu Kibaha Tumbi.
Aliwataka wachezaji hao kujituma kuzingatia yale wanayofundishwa na
walimu wao ili kuhakikisha wanafanya vyema na kutoa wachezaji wazuri
ili kuunda timu ya Kanda inayoundwa na mikoa ya Pwani na Morogoro.
Kwa upande wake ofisa elimu taaluma mkoa wa Pwani Godwin Mkaruka
ambaye aliwakilisha mkoa huo alisema kuwa ana mpongeza mbunge huyo kwa
kuisaidia timu ya mkoa ili iweze kuwakilisha vema mkoa huo.
Aliwataka wadau mbalimbali kujitokeza kuisaidia timu hiyo kwa hali na
mali kama alivyojitolea Mbunge huyo ili iweze kuuletea mkoa ushindi
katika michuano hiyo ambayo hufanyika wilayani humo kila mwaka.
Mwisho.
3 attachments — Download all attachments   View all images   Share all images  
E89A0881.jpgE89A0881.jpg
1311K   View   Share   Download  
E89A0882.jpgE89A0882.jpg
1162K   View   Share   Download  
E89A0874.jpgE89A0874.jpg
1

WANAFUNZI WATAKIWA KULALA ILI WASISIKILIZE WENZAO WAKIFUNDIHSWA

Na John Gagarini, Bagamoyo
SHULE ya Msingi Ludiga wilayani Bagamoyo mkoani Pwani inakabiliwa na uhaba wa madarasa hali ambayo inasababisha baadhi ya wanafunzi wa madarasa mawili kusoma chumba kimoja cha darasa huku wengine wakitakiwa kulala ili wasisikilize wanachofundishwa wenzao.
Akizungumza mbele ya mbunge wa Jimbo la Chalinze Said Bwanamdogo alipotembelea Kijiji cha Talawanda kata ya Talawanda, mwalimu mkuu  msaidizi wa shule hiyo Selestin Casian alisema kuwa shule hiyo ina madarasa matatu tu.
Casian alisema kuwa mbali ya wanafunzi wa madarasa mawili kusomea chumba kimoja pia wanafunzi wengine husomea nje kwenye miti kutokana na upungufu huo wa vyumba vya madarasa.
“Inabidi tuwaambie wanafunzi wa darasa moja walale ili wasisikilize kinachofundishwa na mwalimu ambaye yuko darasani hasa pale mwalimu mwingine anapokuwa bado hajaingia,” alisema Casian.
Aidha alisema kuwa licha ya shule hiyo kuwa na mwaka wa 10 sasa tangu kuanzishwa kwake shule hiyo ina walimu watano ambapo ina jumla ya wanafunzi 320.
“Kwa kweli tunachangamoto kubwa ya madarasa hali ambayo inasababisha wanafunzi kutopatiwa elimu ipasavyo hivyo tunaiomba halmashauri kutusaidia ili tuweze kuepukana na adha hii kwani wanafunzi wanashindwa kusoma vema,” alisema Casian.
Kwa upande wake mbunge wa Bwanamdogo alisema kuwa atapeleka suala hilo halmashauri ili iweze kutatua changamoto hiyo ambayo inakabili baadhi ya shule za Jimbo hilo.
“Changamoto ya madarasa na walimu ni kubwa katika Jimbo la Bagamoyo, lakini kama mnavyojua tatizo kubwa ni fedha kwani halmashauri yetu haina fedha za kutosha hata hivyo tutaendelea kuhimiza ujenzi kwa kushirikiana na wananchi,” alisema Bwanamdogo.
Aliitaka jamii kujitolea kwenye ujenzi wa madarasa na si kuisubiri serikali kwani nayo inakabiliwa na mambo mengi ya kimaendeleo hivyo wahimizane kuchangania kujenga madarasa.
Mwisho.