Wednesday, February 28, 2024

Taasis ya Digital Agenda for Tanzania Initiatives yasisitiza haki ya faragha na ulinzi wa taarifa binafsi Nchini.*


Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Wataalamu kutoka Taasisi ya Digital Agenda for Tanzania Initiative imekutanaa pamoja na wadau kutoka Wizara ya habari, mawasiliano na teknolojia ya habari  wamekutana Jijini Dodoma kujadiliana kuhusu utetezi wa haki kidigitali.

Lengo la kikao hicho ni kutoa matokeo ya ripoti mbili zilizofanywa na Taasisi ya Digital Agenda Tanzania Initiative kuhusu utambuzi Kwa kutumia taarifa za kibayometriki,usajili wa laini za simu unaofanywa na Makampuni ya simu nchini.

Tafiti  imebainisha kuwa makampuni  ya simu nchini licha ya kufanya vizuri katika kutoa huduma lakini bado kuna mapungufu  katika kulinda haki ya faragha na ulinzi wa taarifa binafsi zonazowahusu wateja wao.

Akibainisha mapungufu hayo mkurugenzi mtendaji wa taasisi hiyo Peter Mmbando amesema kuwa ulinzi wa data, uhuru wa kujieleza pamoja na uendeshaji wake vilibainika kuwa ni moja kati ya mapungufu ya mitandao hiyo.

Mmbando amesema kuwa, elimu zaidi Kwa wananchi inapaswa ku ndelea kutolewa ili kuhakikisha taarifa zao zinakuwa salama pamoja na kuhakikisha wanaepukana na makosa ya kimtandao ambayo yamekuwa yakifanyika.

Kwa upande wake  Mtaalamu wa ulinzi wa taarifa binafsi Nchini Tanzania,Mrisho Swetu ameitaka jamii kuamka na kuwa mstari wa mbele katika kulinda taarifa zao. Amesisitiza kuwa taarifa binafsi nyeti za kibayometriki mfano alama za vidole zina athari kubwa endapo zitatumika vibaya.

Pia ameendelea kuhimiza wadhibiti na wachakataji wa taarifa binafsi Nchini kuboresha viwango vya ulinzi wa taarifa binafsi pamoja  na kuendelea kutoa elimu ya ulinzi wa taarifa binafsi kwa mujibu wa sheria ya ulinzi wa taarifa binafsi,2022. Wadhibiti na wachakataji wanapaswa kuheshimu haki ya faragha na hyo itasaidia kuongeza uaminifu na wateja wao.

Kwa upande wa Jamii amesema,wadau wa serikali na sekta binafsi waendelee kutoa elimu kwa umma kuhusu haki ya faragha na ulinzi wa taarifa binafsi.Jamii inapaswa kupewa elimu ya kutosha kuhusu ulinzi wa taarifa binafsi pamoja na haki zao kama haki ya kuomba kufutwa kwa taarifa zako,haki ya kurekebisha,haki ya kupata fidia pale itakapotokea misingi ya sheria ya ulinzi wa taarifa binafsi imekiukwa.

Aidha,ameendelea kusema, mafunzo hayo wamelenga kuyafikia makundi yote katika jamii, mikoa yote ambapo kwa upande wa watu wenye ulemavu wa kuona na kusikia wapo kwenye mpango wa kukutana na wataalamu wa lugha ya alama ili  kujua elimu hiyo itawafikiaje jamii hiyo ya watu wenye ulemavu. 

"Lengo ni kuikumbusha jamii matumizi sahihi  ya taarifa  binafsi,kujua haki zao ,lakini ni muhimu wafahamu kuwa taarifa zao binafsi zikitumika vibaya zinaweza kuleta madhara,lakini wafahamu kuwa endapo kutatokea  uvunjifu wa sheria ya ulinzi wa taarifa binafsi basi ni wapi wanaweza kupeleka malalamiko yao" amesema Mrisho Swetu 

Naye, Afisa Mwandamizi Tume ya Haki za binadamu za Utawara Saidi Zuberi amesema mafunzo hayo yatakwenda  kumasaidia mwananchi kuweza kulinda  taarifa zake na kutambua haki za faragha. 

Pia ametoa wito kwa watoa elimu wa tume ya ulinzi wa data kuwa na miongozo itayoweza kutoa elimu ya haki ya faragha katika jamii .

WATANZANIA WATAKIWA KUENZI FALSAFA ZA MWALIMU JULIUS KAMBARAGE NYERERE






WATANZANIA wametakiwa kuenzi falsafa za Mwalimu Julius Kambarage Nyerere za Ujamaa na Kujitegemea kwani siyo umaskini bali ni kuwafanya wananchi kuwa na umoja ili kujiletea maendeleo.

Hayo yalisemwa na Mwenyekiti wa Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Taifa Paul Kimiti wakati wa Kongamano la Maadili lililofanyika kwenye Shirika la (TATC) Nyumbu Kibaha.

Kimiti alisema kuwa Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alisema kuwa taasisi hiyo ilianzishwa ili kuyaenzi yale aliyoyafanya hasa katika kujitegemea.

"Sisi ambao tunajua alichokuwa akikitaka Nyerere kuhusu uzalendo na kujitegemea na kudumisha umoja na amani lazima tuwakumbushe viongozi na vijana ili wazingatie falsafa hizo ili kuleta maendeleo,"alisema Kimiti. 

Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Kikosi cha Nyumbu na Mkurugenzi wa Nyumbu Kanali Charles Kalambo alisema Shirika hilo ambalo ni maono ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere limepata mafanikio ikiwa ni pamoja na kubuni gari aina ya Nyumbu.

Kalambo alisema kuwa wanamshukuru Rais Dk Samia Suluhu Hassan kwa kulipatia Shirika la Nyumbu fedha kwa ajili ya kufanya shughuli zake mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuendeleza miradi ya kiufundi.

Naye Kanali Ngemela Lubinga katibu mkuu mstaafu (NEC-CCM) siasa na uhusiano wa kimataifa akifundisha somo la uzalendo, itifaki na uadilifu alisema kuwa viongozi wanapaswa kuwa na moyo wa kujituma kwani ndiyo msingi wa kujenga jamii bora na yenye uzalendo.

Lubinga alisema kuwa viongozi wanapaswa kuwa na uadilifu ili kujenga jamii bora pia wawe wabunifu, moyo wa kujituma ili kuleta maendeleo kwa wananchi na awajali ili kuwa na mipango ya pamoja.

Balozi Mstaafu Meja Jenerali Anselm Bahati alisema kuwa ili kuwa na usalama mahali pa kazi kwa wafanyakazi lazima wafanyakazi wapate mafunzo ya namna ya kujilinda na kujikinga.

Bahati alisema kuwa wafanyakazi wakiwa na mazingira salama watakuwa na uwezo wa kuzalisha pia maslahi yao kuangaliwa ili kuepukana na afya ya akili inayotokana na msongo wa mawazo.

Naibu Katibu Mkuu wa Taasisi hiyo Neema Mkwachu alisema malengo ni kutoa elimu kwa wanafunzi kuanzia ngazi ya shule za msingi hadi vyuo juu ya falsafa za Nyerere ikiwemo uzalendo wa nchi.

Mkwachu alisema kuwa pia ni kuwa na klabu za Mwalimu Nyerere ambazo zitakuwa zinatakuwa pia na uwezo wa kutunza mazingira ambayo ni moja ya vitu alivyohimiza Hayati Nyerere 

Katibu wa Taasisi ya Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere Mkoa wa Pwani Abdul Punzi alisema kuwa ili kuenzi falsafa za Nyerere kwa kufungua Klabu ya Mwalimu Nyerere Nyumbu.

Punzi alisema kuwa uzalendo unapaswa kuanzia chini kabisa ili wananchi watambue misingi mizuri iliyoasisiwa na Nyerere na kuifanya Tanzania kuwa na umoja na mshikamano ambapo kongamano hilo lilidhaminiwa na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Benki ya CRDB na NSSF.


Monday, February 26, 2024

*HISTORIA YAANDIKWA; JNHPP YAINGIZA MEGAWATI 235 GRIDI YA TAIFA*

📌 *Serikali yatekeleza ahadi kabla ya siku tatu*

📌 *Megawati 235 nyingine kuingizwa Machi, 2024*

📌 *Uzinduzi rasmi kufanyika mwezi Machi mwaka huu*

📌 *Dkt. Biteko asema hakuna kulala; vyanzo vipya kutekelezwa*

📌 *Mkandarasi apongeza usimamizi wa Dkt.Biteko*

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amesema kuwa, mradi wa umeme wa Julius Nyerere (JNHPP) wenye uwezo wa megawati  2,115  umeanza kazi na kuingiza  megawati 235 katika gridi ya Taifa kupitia mtambo Namba 9. 

Hatua hii ni utekelezaji wa ahadi ya Serikali kuwa mtambo huo ungeanza kuzalisha umeme tarehe 25 Februari 2024, ahadi iliyotimizwa siku tatu kabla kuanzia tarehe 22 Februari 2024  mtambo huo ulipoanza uzalishaji.

Dkt. Biteko amesema hayo tarehe 25 Februari 2024 wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo kwa baadhi ya wakuu wa vyombo vya Habari na Wahariri katika eneo la mradi wilayani Rufiji mkoani Pwani ambapo wahariri hao walipata fursa ya kutembelea maeneo mbalimbali ikiwemo Bwawa la kuhifadhi maji yatakayozalisha umeme, Tuta Kuu na mitambo ya umeme.

Ameeleza kuwa, kuingia kwa megawati 235 kwenye Gridi ya Taifa  kumeboresha hali ya upatikanaji umeme nchini na kupunguza upungufu wa umeme kwa zaidi ya asilimia 85.

Ameongeza kuwa, utekelezaji wa mradi wa Julius Nyerere unaendelea na ifikapo mwezi  Machi 2024 megawati nyingine 235 zitaingia katika gridi kupitia mtambo namba 8 na kufanya JNHPP kuingiza megawati 470 kwenye gridi na hivyo kupelekea nchi kuwa na ziada ya umeme ya megawati 70.

Amesema utekelezaji wa mradi huo ni jitihada za Rais, Dkt.Samia Suluhu Hassan ambaye alikuta mradi huo ukiwa na aslimia 33 na sasa  mradi huo unafikia mwisho.

Amesema, Dkt. Samia anaijali nchi kwa dhati na sasa mipango yake ya maendeleo haiangalii kipindi cha sasa tu bali miaka 30 hadi 40 ijayo na ndio maana ameshaagiza uendelezaji wa vyanzo vipya vya umeme ikiwemo Gesi, Maji na Nishati Jadidifu inayojumuisha Jua, Upepo na Jotoardhi.

Dkt. Biteko pia amepongeza juhudi za Serikali ya  Awamu ya Tano chini ya Hayati, Dkt. John Pombe Magufuli kwa uamuzi wa kutekeleza mradi huo ambao ulianza kutekelezwa mwaka 2018.

Katika hatua nyingine, Dkt. Biteko ameeleza kuwa, utekelezaji wa JNHPP hauifanyi Wizara ya Nishati na Taasisi zake kubweteka na kutegemea umeme kutoka mradi huo pekee bali kasi ya utekelezaji wa miradi mingine mipya inaendelea ikiwemo mradi wa Rumakali (222MW), Ruhudji (358) na miradi ya Jotoardhi ya Ngozi na Kiejo-Mbaka pamoja na mradi wa umeme Jua wa Kishapu (150MW).

Kuhusu utunzaji wa mazingira, Dkt. Biteko ametoa wito kwa Wahariri wa Vyombo vya Habari kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa utunzaji wa mazingira ambao ndio unasababisha mabwawa ya umeme kuwa na maji ya kutosheleza kuzalisha umeme na pia kutoa elimu kuhusu athari za kuharibu vyanzo vya maji vinavyopeleka maji pia katika mabwawa ya umeme.

Kwa wananchi wanaozunguka maeneo  yenye mitambo ya kuzalisha umeme, Dkt. Biteko amesisitizaTANESCO ihakikishe hawapati changamoto ya umeme kwani hao ndio walinzi wa maeneo hayo na mradi unapofika katika eneo lolote lazima ubadilishe hali ya wananchi katika eneo husika kwa namna mbalimbali ikiwemo uboreshaji wa huduma za kijamii.

Dkt. Biteko ameipongeza TANESCO na  kampuni ya usimamizi wa mradi ya TECU kwa utekelezaji na usimamizi madhubuti wa mradi ambao umewezesha kuingiza megawati 235 kwenye gridi.

Kwa upande wake, Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso amesema kuwa, ujazo wa maji unaohitajika katika Bwawa la umeme la JNHPP ni mita za ujazo bilioni 32.7 na sasa kuna mita za ujazo bilioni 28 hivyo bado mita nne tu Bwawa hilo kujaa kabisa.

Amesema kuwa, makadirio ni kuwa mita nne zilizobaki zitajaa mwezi huu kupitia usimamizi madhubuti wa Bonde la Maji la Rufiji.

Ametoa wito kwa wananchi kutunza vyanzo vya maji na kutofanya uharibifu wa mazingira na vyanzo vya maji pia wasichepushe maji kiholela.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Abubakar Kunenge amesema kuwa, mradi huo ni muhimu katika kutekeleza dhamira ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuifanya Pwani kuwa Mkoa wa kimkakati kwa kujenga viwanda vingi zaidi ambavyo kufanya kwake kazi kunategemea nishati ya umeme ya uhakika.

Amesema kuwa, mahitaji ya umeme mkoani Pwani ni megawati 130 lakini bado hayatoshelezi mahitaji hivyo mradi wa JNHPP kupitia kituo cha umeme cha Chalinze kitawezesha Mkoa huo kupata umeme wa uhakika ambao utachochea wawekezaji wapya.

Ameongeza kuwa, kwa sasa Mkoa wa Pwani una viwanda 1,533 ambapo  katika Serikali ya Awamu ya Sita viwanda 30 vinajengwa huku 17 vikiwa ukingoni kumalizika hivyo mradi wa JNHPP ni muhimu katika kufanya viwanda hivyo kufanya uzalishaji.

Meneja Mradi kutoka kampuni zinazotekeleza mradi huo (Arab Contractors na Elsewedy Electric) Mohamed Zaky, amesema kuwa kampuni hiyo inaona fahari kufikia hatua hiyo ya uzalishaji na kwamba nia yao ni kutimiza ndoto ya Tanzania kuzalisha megawati 2115 kupitia mradi wa JNHPP.

Aidha, amempongeza Dkt. Doto Biteko kwa msukumo anaoutoa kwa wakandarasi hao ili kutekeleza mradi kwa wakati na pia kwa kuusimamia kwa karibu mradi husika.

Viongozi wengine walioambatana na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati ni  Mkuu wa Wilaya ya Rufiji, Meja Edward Gowele, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba, Naibu Katibu Mkuu Mteule Wizara ya Nishati, Dkt. James Mataragio, Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga,  Mwenyekiti wa Bodi ya TANESCO, Dkt. Rhimo Nyansaho na Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mhandisi Gissima Nyamo-Hanga.

Sunday, February 25, 2024

TAASISI YA KUMBUKUMBU YA MWALIMU JULIUS KAMBARAGE YATOA MAFUNZO ITIFAKI, UZALENDO NA USALAMA MAHALI PA KAZI KWA CWT KIBITINYERERE







TAASISI ya kumbukumbu ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Mkoa wa Pwani imetoa mafunzo ya Itifaki, Uzalendo na Usalama Mahali pa kazi kwa viongozi wa walimu wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti na kuzindua Club ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Wilaya ya Kibiti.

Mafunzo hayo yalitolewa Februari 24, 2024 Wilayani Kibiti kwa viongozi walimu hao kutoka Chama Cha Walimu (CWT) Wilaya ya Kibiti wapokea mafunzo ya ya Itifaki, Uzalendo na Usalama yalifunguliwa na Bi Nelea Nyanguye  ofisa Usalama mahali pa kazi wa Chama Cha Walimu (CWT) Taifa.

Katibu wa Taasisi hiyo ya Kumbukumbu ya Mwalimu Julius Nyerere Mkoa wa Pwani Ndugu Omary Punzi alifundisha mada ya Itifaki na Uzalendo na kuwaelekeza misingi ya Kiitifaki na kuwa Mzalendo wa Taifa la Tanzania.

Sadick Mchama alifundisha Usalama Mahali pa kazi ambapo mgeni rasmi Ndugu Salumu Mzanganya ofisa Tarafa Kibiti ambaye  alimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Kibiti Mheshimiwa Kanali Joseph Kolombo, alitoa nasaha kwa wahitimu kuwa baada ya Mafunzo hayo kuwa wanatakiwa wawe wazalendo na kuisidia Wilaya, Mkoa na Taifa kwa ujumla kisha alizindua Club ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Wilaya ya Kibiti.

Kwa Upande wa Mwenyekiti wa CWT  Wilaya ya Kibiti Ndugu Hamdani Juma na Katibu Wake Bi Crencencia Ditrick walipongeza na kushukuru kuletewa mafunzo ambapo jumla ya washiriki 130 waliopatiwa vyeti vya mafunzo na  hayo.

NEC YATOA VIBALI VYA ELMU YA MPIGA KURA NA WATAZAMAJI WA UCHAGUZI MDOGO WA UDIWANI KATA 23.

 

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) katika kikao chake cha tarehe 24 Februari, 2024, kilichofanyika katika Ofisi za Tume Jijini Dodoma imetoa vibali vya kutoa elimu ya mpiga kura wakati wa uchaguzi mdogo wa Udiwani katika kata 23 za Tanzania Bara utakaofanyika tarehe 20 Machi, 2024 kwa asasi za kiraia 11.

Kwa Mujibu wa Taarifa kwa Vyombo vya Habari iliyosainiwa na Mkurugenzi wa Uchaguzi Kailima, R. K imeainisha Asasi za kiraia 11 ambazo zimekidhi vigezo na kupewa vibali vya kutoa elimu ya mpiga kura pamoja na kata walizoomba kutoa elimu  hiyo kuwa ni Mbogwe Legal Aid Organization (MBOLAO) Isebya iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe, Sustainable Hub for Policy Initiatives (SHPI) Mshikamano iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Musoma.

Asasi zingine ni Promotion and Women Development Association (PWDA) Kasingirima iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma/Ujiji, Bagamoyo Community Capacity Empowerment and Education (BCCEE) Fukayosi iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Action for Democratic Governance (A4DG) Kimbiji iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni.

Asasi zingine ni Vanessa Foundation ambayo itatoa elimu katika kata ya Nkokwa iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kyela, Tanzania Centre for Disability Development Initiatives (TCDDI) Nkokwa iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kyela, Safe Society Platform Tanzania (SSPT) Busegwe iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Butiama na Isebya iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe

Asasi zingine za kiraia zilizopata kibali ni Youth Against Aids and Poverty Association (YAAPA) ambayo itatoa elmu katika kata ya Kasingirima iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma/Ujiji, Musoma Municipal Paralegal Organisation (MMPO) Mshikamano iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Musoma.

Asasi nyingine iliyopata kibali ni Shirika la Elimu ya Uraia na Uzalendo “Civic Education and Patriotism Association” iliyoomba kutoa Elimu katika kata za Kimbiji iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni, Msangani iliyopo katika Halmashauri ya Mji Kibaha, Fukayosi iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Mlanzi iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti na Kibata iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa.

Wakati huo huo, Tume pia imetoa kibali kwa asasi za kiraia tatu ambazo zimekidhi vigezo ili ziweze kutazama uchaguzi mdogo wa Udiwani katika Kata 23 za Tanzania Bara.

Asasi hizo tatu zitakazoenda kutazama uchaguzi Mdogo wa udiwani siku ya Jumatano tarehe 20 Machi, 2024 ni Tanzania Alliance for Disability Development Initiatives itakayokuwa katika kata ya Mhande iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba, Bridge Development Trust Organisation itakuwa katika kata ya Buzilasoga iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema na Promotion and Women Development Association itayokuwa katika Kata ya Kasingirima iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma/Ujiji.

Aidha, katika kikao hicho, Tume imezitaka asasi za kiraia zilizopata kibali cha kutoa elimu ya mpiga kura, kuzingatia Mwongozo wa Elimu ya Mpiga Kura wa Mwaka 2020 katika kipindi chote cha kutoa elimu hiyo katika uchaguzi mdogo.

MAMA KOKA AFANYE KWELI AGAWA DOTI ZA VITENGE KUELEKEA SIKU YA MWANAMKE DUNIANI

 

NA MWANDISHI WETU

Mke wa Mbunge wa  Jimbo la Kibaha Mjini Selina Koka  amegawa doti za  sare 125 za vitenge  kwa ajili ya sherehe za maadhimisho ya siku ya  Mwanamke Duniani zilizogharimu kiasi cha shilingi milioni 2.

Sare hizo ambazo zimegawiwa katikka makundi mbali mbali ikiwemo Jumuiya ya wazazi, Wajumbe wa Baraza la UWT Kibaha Mjini, Wajumbe Wanawake wa Baraza la Wazazi la Wilaya, Wajumbe wanawake wa Baraza la UVCCM Kibaha Mjini Pamoja na Wajumbe Wanawake wa Halmashauri kuu ya CCM Wilaya Kibaha Mjini. 

Akikabidhi sare hizo kwa niaba ya Mama Selina Koka Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Kibaha mji Method Mselewa  amesema huu ni Utaratibu wa Ofisi ya Mbunge kupitia kwa Mama Koka kugawa sare kwa wanawake kila mwaka na kila zinapofika Sherehe hizo pamoja na Makongamano mbalimbali. 

Kwa Upande wake Mama Selina Koka akizungumza katika mahojiano maalumu kwa njia ya simu alisema kwamba ameamua kutoa sare hizo kwa lengo la kuungana na wanawake wenzake katika kusherekea kwa pamoja siku hiyo.

"Nimetoa sare zipatazo 125 kwa ajili ya  makundi mbali mbali ya wanawake,ikiwemo kundi la Uwt,Uvccm,Wazazi,pamoja na chama chenyewe cha Ccm  ambapo wao ndio watawakilisha wanawake wengine wote wa Jimbo la Kibaha mjini,"alisema Selina Koka.

Mama Koka alisema kwamba amekuwa akishirikiana bega kwa bega na wanawake wenzake katika mambo mbali mbali ya kijamii ambayo yamekuwa yakifanyika ikiwemo hili la kuelekea maadhimisho ya siku ya wanawake duniani.

Pia aliahidi kuendelea kushirikiana kwa dhati na wanawake wenzake na kuwatakia kila la kheri katika sherehe hizo ambazo kiwilaya zinatarajiiwa kufanyika machi 5 mwaka huu mjini Kibaha.

Mama Koka  alifafanua kwamba ameamua kutumia jumuiya  hizo ikiwa kama wawakilishi wa wanawake wengine wote wa Jimbo zima  la Kibaha mjini kwani sio rahisi kwa kila mmoja kupata sare hiyo kwa ajili ya sherehe hizo.

Katika hatua nyingine amesema kwamba anawapenda wanawake wote na kwamba wajitokeze kwa wingi siku hiyo kwa ajili ya kusherekea siku yao ambayo ni muhimu kwa ajili ya kuonana na kubadilishana mawazo.

Naye Mwenyekiti wa Jumuiya ya umoja wa wanawake (UWT) Wilaya ya Kibaha Mjini Elina Mgonja amemshukuru kwa dhati Mama Koka pamoja na  Mbunge kwa kujali wanawake wa Kibaha na kwamba tunapaswa kumtia moyo.

Mgonja alisema kwamba wanawake wa Kibaha wamepata Mama ambaye amekuwa ni mstari wa mbele katika kusaidia mambo mbali mbali ya kijamii pamoja hivyo anastahili sifa  na kumthamini.

"Kwa kweli  tumefarijika sana kupokea sare hizi za vitenge kiukweli mama Selina koka ni mfano wa kuigwa kutokana na kuonyesha mashirikiano na mahusiano mema katika kila jambo,"alisema Mgonja.

Aidha Mwenyekiti Mgonja alisema kwamba Mama koka amekuwa ni kichocheo kikubwa katika kila nyanja ikiwepo sambamba na kuwawezesha wanawake kiuchumi kwa kuwapatia mitaji na fedha.

Naye Katibu wa UWT Cecilia Ndalu amesema kuwa kitendo cha Mama Koka kujali wanawake ni kitendo cha kipekee sana  kwani kuwa mke wa Mbunge hawajibik kwa wanawake moja kwa moja lakini amejigusa na kujali sana. 

Wajumbe wengi waliopokea sare hizo wameendelea kuishukuru familia ya Mhe Koka kwa kujitoa na wameahidi kuendelea kumuunga mkono Mhe Koka katika kuhakikisha shughuli zake za utekelezaji wa ilani unaenda vyema. 

Sherehe za Mwanamke zinaadhimishwa Duniani kote na kwa upande wa  Kibaha Mjini kilele kitakuwa siku ya tarehe 05/03/2024 katika viwanja vya Mailimoja. 



        MWISHO

Saturday, February 24, 2024

SHULE YA EL-SHADDAI YAWASHIKA MKONO WATHIRIKA WA MAAFA HANANG.

 

NA MWANDISHI WETU, DODOMA

UONGOZI wa shule ya Msingi  El shaddai  iliyopo Dodoma umekabidhi misaada ya kibinadamu ikiwemo mchele, unga, maharagwe, nguo, dawa za meno na vyombo mbalimbali vya kupikia kwa ajili ya waathirika wa maafa ya maporomoko ya tope, mawe na miti kutoka mlima Hanang’ yaliyotokea tarehe 3 Disemba 2024 mkoani Manyara.

Akipokea misaada iliyotolewa na shule hiyo tarehe 23 Februari, 2024 kwaniaba ya Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi,  Kaimu Mkurugenzi Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Bi. Jane Kikunya amesema Ofisi inatambua mchango mkubwa wa Taasisi zinazoendelea kushiriki katika kurejesha hali kwa waathirika wa maafa hayo kwa namna wanavyoendelea kutoa misaada mbalimbali ili kusaidia hatua ya urejeshaji hali inayoendelea.

"kipekee kwa niaba ya Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu naomba kuwashukuru kwa moyo mliouonesha na nia katika kuchangia na kutoa msaada kwaajili ya waathirika wa maafa, tunashukuru kwa Shule yenu kwa kujitokeza na kuchangia misaada muhimu kwaajili ya waathirika wa Hanang, misaada iliyotolewa itawafikia waathirika wote kwa utaratibu uliowekwa na Ofisi."alisema Bi. Jane Kikunya.

Alieleza kuwa Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wameendelea kurejesha hali za waathirika wa maafa hayo yaliyosababisha vifo, uharibifu wa makazi, miundombinu ya barabara, umeme na mashamba, huku akitoa wito kwa wadau kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali katika kufanikisha hatua zilizopo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Shule hiyo  Bi. Juliana Kallinga amesema uongozi wa shule na wafanyakazi wa shule hiyo wameandaa baadhi ya vitu ambavyo ni ishara ya kuwafariji waathirika hao.

"Kama familia ya El-Shaddai tunapenda kuwafariji Watanzanaia wenzetu walioathirika kwa kuwapatia msaada wa vitu mbalimbali ikiwemo mchele, unga, maharagwe, nguo mbalimbali kwa wakubwa na wadogo, dawa za meno na vyombo mbalimbali vya kupikia,lakini pia tunamuomba Mungu aendelee kuwapa mfaraja na nguvu kila aliyepotelewa na ndugu jamaa na marafiki, hakika shule yetu iliguswa na changamoto hii."alisema Bi. Juliana.




CAPTIONS


P 1.

Kaimu Mkurugenzi Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Bi. Jane Kikunya akizungumza mara baada ya kupokea msaada ya kibinadamu kutoka kwa uongozi pamoja na walimu wa shule ya Msingi El-shaddai Februari 23, 2024 Jijini Dodoma.



P 2.

Mkurugenzi wa Shule ya Msingi  El-shaddai Bi. Juliana Kallinga akisoma taarifa ya msaada waliyoitoa kwa waathirika wa maporomoko ya tope, mawe na miti Wilaya ya Hanang’ mkoani Manyara.



P 3.

Mkurugenzi Idara ya Uwezeshaji Kiuchumi na Maendeleo ya Sekta Binafsi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Bw. Condrad Millinga akipokea taarifa msaada iliyosomwa na Mkurugenzi wa Shule ya Msingi  El-shadai Bi. Juliana Kallinga.


P 4.

Baadhi ya vitu vilivyopokelewa ikiwemo mchele, unga, maharagwe, nguo, dawa za meno na vyombo mbalimbali vya kupikia kwa ajili ya waathirika wa maafa ya maporomoko ya tope, mawe na miti kutoka mlima Hanang’.


(PICHA ZOTE NA OFISI YA WAZIRI MKUU)