Monday, April 3, 2017

WATUHUMIWA UHALIFU WALIOVALIA HIJABU WAUWAWA NA POLISI

Na John Gagarini, Kibaha
WATU watatu waliokuwa wamepakizana kwenye pikipiki moja wanaodhaniwa kuwa ni wahalifu wakiwa wamevalia hijabu wameuwawa kwa kupigwa risasi na polisi baada ya kukaidi amri ya kutakiwa kusimama.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Kibaha Kamanda wa Polisi mkoani Pwani Onesmo Lyanga alisema kuwa pikipiki nyingine mbili zilifanikiwa kukimbia.
Lyanga akielezea juu ya tukio hilo alisema kuwa lilitokea Aprili 2 mwaka huu majira ya saa 12:00 mchana eneo la kizuizi cha Mwembe Muhoro wilaya ya Rufiji mkoani Pwani barabara kuu ya Dar es Salaam Lindi.
“Siku ya tukio askari walipata taarifa kuwa kulikuwa na pikipiki tatu zikitokea Kibiti kwenda mikoa ya Kusini zikiwa zimebeba watu watatu kila moja huku miongoni mwa pikipiki hizo kati yake mbili wamebebwa watu waliovaa hijabu,” alisema Lyanga.
Alisema kuwa askari wa barabarani walipewa taarifa katika kizuizi cha Mparange na kuwasimamisha ili wawahoji lakini walikataa na kupita ambapo waliwajulisha wenzao kwenye kizuizi cha Ikwiriri lakini walikaidi kusimama.
“Baada ya hapo walifika kizuizi cha Ikwiriri lakini bado walikaidi kusimama na kuendelea kukimbia ndipo walipofika kituo cha Muhoro hata hivyo hawakusimama na askari waliokuwa doria wakiwa kwenye gari waliwafuatilia wakijaribu kuwafuatilia na wakavuka daraja la Mkapa na waliwapa onyo kwa kupiga risasi hewani,” alisema Lyanga.
Aidha alisema kuwa baada ya hapo watu hao waliruka kwenye pikipiki na kuanza kukimbilia msituni na ndipo askari walipowapiga risasi za miguu na kiunoni na kufanikiwa kuwakamata.
“Majeruhi hao walijulikana ni wanaume hata hivyo majina yao hayakuweza kufahamika na walikuwa kwenye pikipiki yenye namba za usajili MC 272 BLW aina ya Boxer yenye rangi nyeusi ambapo watu hao wanaodhaniwa kuwa ni wahalifu kwa mwonekano wao walijaribu kuwawahisha Hospitali ya Misheni ya Mchukwi,” alisema Lyanga.
Lyanga alisema kuwa walipofikishwa hospitali daktari alithibitisha kuwa watu hao wamefariki dunia ambapo hata hivyo majina yao hayakuweza kufahamika huku pikipiki nyingine mbili zilitoroka na kuelekea mkoa wa Lindi na taarifa zimetolewa polisi ili wawakamate.
Aliwataka wananchi kuwa watulivu pale wanaposimamishwa na askari polisi badala ya kujaribu kutoroka na kwa sasa jeshi hilo limeimarisha doria katika kukabiliana na uhalifu.
Mwisho.