Friday, October 21, 2016

WALIBYA WASAIDIA MRADI WA MAJI MKURANGA


Na John Gagarini, Mkuranga

WANANCHI wametakiwa kuwa na utamaduni wa kulipa kodi mbalimbali za serikali ili ziweze kutumika kwa ajili ya maendeleo kama wanavyofanya wananchi wa Libya.

Hayo yalisemwa wilayani Mkuranga na mkurugenzi wa Taasisi ya World Islamic Call Society iliyopo chini ya ubalozi wa Libya hapa nchini Ammara Zaiyani wakati akikabidhi mradi wa kisima cha maji kwenye Kijiji cha Binga–Kisiju.

Zaiyani alisema kuwa fedha ambazo zimesaidia ujenzi wa kisima hicho cha maji ya kunywa chenye thamani ya shilingi milioni 18 zimetokana na kodi za wananchi wa Libya kwa ajili ya kusaidia watu wenye changamoto mbalimbali za kimaendeleo.

“Wananchi wa Libya wanajitolea kuwasaidia wenzao hivyo na nyie mnapaswa kuwa na utamaduni wa kuwasaidia wengine kupitia kwenye malipo mbalimbali ya serikali yenu ambayo ina sema hapa Kazi Tu,” alisema Zaiyani.

Naye mwakilishi wa Ubalozi wa Libya hapa nchini Mohamed Atoumi alisema kuwa serikali ya Libya kupitia taasisi hiyo imekuwa ikipokea maombi mbalimbali na imekuwa ikisaidia kadiri ya uwezo unapokuwepo.

Atoumi alisema kuwa wamekuwa wakisaidia kwenye sekta mbalimbali ikiwa ni pamoja kwenye huduma za afya, maji na shughuli nyingine za maendeleo lengo likiwa ni kudumisha ushirikiano uliopo na Tanzania.

Kwa upande wake kadhi mkuu wa mkoa wa Pwani Sheikh Hamis Mtupa alisema kuwa wanashukuru kwa msaada huo kwani umesaidia kuwaondolea adha wananchi wa Kijiji hicho ambao walikuwa wakishinda wakitafuta maji ambayo siyo safi wala salama.

Mtupa alisema kuwa wananchi wanapaswa kulinda miundombinu ya kisima hicho ili isiharibike kwani maji hayo ni kwa wananchi wote bila ya kujali dini ya mtu na ni huduma muhimu kwa binadamu.

Naye mkazi wa kijiji hicho Mwanahawa Maulid alisema kuwa wamekuwa wakihangaika kutafuta maji ambayo yanapatikana mbali na wamekuwa wakitumia muda mwingi kusubiria maji.

Maulid alisema kuwa maji waliyokuwa wakiyatumia ni ya kuchimba chini ambayo si salama kiafya na yamekuwa wakiwasababishia magonjwa mbalimbali kama vile kuhara na UTI.

Mwisho.





Mkurugenzi wa Taasisi ya World Islamic Call Society ya Libya tawi la Tanzania Ammara Zaiyani kulia aliyeshika ndoo ya maji baada ya kumtwisha ndoo ya maji Saida Ally mkazi wa Kijiji cha Binga-Kisiju kata ya Dondo wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani, kushoto kadhi mkuu wa mkoa wa Pwani Sheikh Hamis Mtupa (Picha na John Gagarini)
Mkurugenzi wa Taasisi ya World Islamic Call Society ya Libya tawi la Tanzania Ammara Zaiyani katikati akielezea jambo kulia ni kadhi mkuu wa mkoa wa Pwani Sheikh Hamis Mtupa na kushoto ni mwakililishi wa balozi wa Libya Mohamed Atoumi wakati wa uzinduzi wa mradi wa maji kwenye Kijiji cha Binga Kisiju- kata ya Dondo wilaya ya Mkuranga mkoa wa Pwani Picha na (John Gagarini)

Mkurugenzi wa Taasisi ya World Islamic Call Society ya Libya tawi la Tanzania Ammara Zaiyani akifungua bomba la maji baada ya uzinduzi wa kisima cha maji kwenye Kijiji cha Binga-Kisiju wilayani Mkuranga mkoani Pwani kushoto kwake ni mwakililishi wa balozi wa Libya Mohamed Atoumi (Picha na John Gagarini)  

      

Monday, October 3, 2016

MWANAMKE ATUMIKA WIZI CWT WALINZI WAWILI WASHIKILIWA

Na John Gagarini, Kibaha

JESHI la la polisi mkoani Pwani linawashikilia walinzi wawili wa jengo la ofisi ya Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) mkoa baada ya watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi kuvunja na kuiba fedha kiasi ambacho bado hakijajulikana na computer za ofisi hizo.

Akizungumzia na waandishi wa habari mjini Kibaha kuhusiana na tukio hilo katibu wa (CWT) Nehemiah Joseph amesema kuwa tukio limetokea usiku wa octoba mosi kuamkia octoba 2 mwaka huu.

Joseph amewataja walinzi hao kutoka kampuni ya Noble security Tanzania Ltd ya Kibaha kuwa ni Hamad Kisoki (32) mkazi wa Maili Moja na Said Mohammed (39) mkazi wa Mwanalugali.

Amesema siku ya tukio walinzi waliotakiwa kuingia zamu walikuwa ni wawili lakini Said Mohammed pekee ndiye aliyefika kazini na mwenzake Hamad Kisoki haikuweza kufahamika mara moja ni kwa sababu gani hakuingia kazini.

Aidha amesema kuwa Said Mohamed alipokuwa kwenye lindo lake anadaiwa kupatiwa chips na juisi vinavyosemekana kuwa na madawa ya kulevya kutoka kwa mwanamke asiyefahamika.

Katibu huyo wa CWT mkoa wa Pwani ameeleza kuwa baada ya kupatiwa chakula hicho mlinzi alipoteza fahamu na hivyo kutoa mwanya kwa watu hao kuvunja milango ya ofisi hizo na kuingia na kuiba vitu hivyo ambavyo thamani yake bado haijafahamika.

Ametaja ofisi zilizopo kwenye jengo hilo ambazo zimeibiwa ni pamoja na CWT mkoa ,CWT wilaya,beem financial services (BFS) ,Chodawu,Tuico na TCCIA ambapo kwasasa wameshafikisha taarifa hizo polisi kwa hatua zaidi na ofisi ya chama hicho imeshakaa na taasisi zote zilizopanga jengo hilo kufanya tathmini.

hata hivyo amesikitishwa sana kutokea kwa wizi huo na kushangazwa na mlinzi huyo kula ama kununua vyakula kwa watu wasiowajua kwani kwa kufanya hivyo kumesababisha kuwapa wahalifu urahisi kutekeleza tukio hilo ambalo limesababisha hasara kwa wamiliki wa ofisi hizo.

Kwa upande wake kamanda wa polisi mkoani Pwani,Bonaventure Mushongi ,amekiri kutokea kwa tukio hilo ambapo amesema taarifa ya tukio hilo ilitolewa  saa 5 asubuhi kutoka kwa Elizabeth Thomas ambae ni katibu wa chama CWT wilaya ya Kibaha huko mkoani A ,kata ya Tumbi.

Mushongi amesema kuwa baada ya kufanya wizi huo watu hao walitokomea kusikojulikana na jeshi hilo bado linawatafuta,huku akiomba ushirikiano kwa wananchi kuwafichua watu wanaowadhania kuhusika na wizi huo na kwasasa wanawashikilia walinzi hao kwa ajili ya uchunguzi juu ya tukio hilo.

Mwisho