Saturday, September 9, 2017
Wednesday, September 6, 2017
WATATU WAFA WAKITOKA BUNGENI DODOMA KUSHUHUDIA KUAPISHWA WABUNGE VITI MAALUMU CUF
Na John
Gagarini, Kibaha
WATU
watatu wamefariki dunia huku wengine watatu wakijeruhiwa walipokuwa wakitokea
Bungeni mkoani Dodoma kushuhudia kuapishwa kwa wabunge saba wa Viti Maalumu wa
Chama Cha Wananchi (CUF) baada ya gari walilokuwa wakisafiria kugongana na lori
la mizigo.
Hayo
yalisemwa mjini Kibaha na kamanda wa Polisi mkoani Pwani Jonathan Shana
alipozungumza na waandishi wa habari na kusema kuwa watu hao walifia papo hapo.
Kamanda
Shana alisema kuwa tukio hilo lilitokea Septemba 6 majira ya saa 8:30 usiku
eneo la Kijiji cha Ubena Zomozi barabara ya Dar es Salaam-Morogoro wilaya ya
Kipolisi Chalinze-Bagamoyo.
“Gari
lililokuwa limetoka Dodoma kwenda Muheza mkoani Tanga ni aina ya Toyota Noah
lenye namba za usajili T 968 CSK likiendeshwa na dereva Uled Sarumaa (32) mkazi
wa Muheza liligongana na gari aina ya Scania lenye namba za usajili T 929 CBK
lenye tela namba T 472 CAX lililokuwa likiendeshwa na Yasin Kanoni (35) mkazi
wa Jijini Dar es Salaam na kusababisha vifo hivyo,”alisema Shana.
Aliwataja
waliokufa kwenye ajali hiyo kuwa ni dereva wa Noah Sarumaa, Mary Komba (40)
mkulima mkazi wa Muheza na mtu aliyetambuliwa kwa jina moja la Isaack
mfanyabiashara anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka (37).
“Majeruhi
wa ajali hiyo kuwa ni Juma Nindi (47) mfanyabiashara wa Muheza, Chausiku Hassan
(47) mkulima wa Muheza na Ester Mafie (67) mkulima mkazi wa Muheza,” alisema
Shana.
Aidha
alisema kuwa miili ya marehemu imehifadhiwa kwenye Hospitali Teule ya Rufaa ya
mkoa wa Pwani Tumbi kusubiri uchunguzi wa daktari na kusubiri ndugu kwa ajili
ya mazishi huku majeruhi wakiwa wamelazwa kituo cha afya cha Chalinze
Alibainisha
kuwa na chanzo cha ajali kinachunguzwa na alipoulizwa juu ya waliokufa kama ni
viongozi wa CUF amesema kuwa bado hajapata taarifa kuhusiana na hilo pia dereva
wa lori Yasin Kanoni alikimbia mara baada ya tukio hilo na kwa sasa anatafutwa.
Mwisho.
BABA WA KAMBO AMJERUHI MTOTO KWA KUIBA MAYAI MAWILI
![]() |
Mtuhumiwa Abdala Machupa akiwa kituo cha Polisi Kongowe |
Na John
Gagarini, Kibaha
JESHI la
Polisi Mkoani Pwani linamshikilia Abdala Machupa (49) fundi ujenzi mkazi wa Kongowe
kwa tuhuma za kumjeruhi kwa kumkata na kisu kichwani mwanae wa kufikia (jina limehifadhiwa) mwenye umri wa miaka (5) mwanafunzi wa shule ya awali ya Kongowe Kati kwa
madai ya kuiba mayai mawili.
Kwa
mujibu wa taarifa zilizotolewa na kamanda wa Polisi mkoani humo Jonathan Shana
alisema kuwa mtuhumiwa huyo alipata taarifa hizo mitaani za mwanae kuiba mayai hayo.
Kamanda
Shana alisema kuwa mtoto huyo alitutuhumiwa
kuiba mayai kwa Bibi Baby Septemba 4 majira ya saa 2 usiku na kumfiki mama yake
mzazi aliyefahamika kwa jina moja la Hadija ambaye alimkanya mwanae kwa
kumchapa viboko.
“Mnamo
Septemba 5 mtuhumiwa huyo alipata taarifa mtaani kuwa mtoto wake kaiba mayai
alirudi nyumbani na kuanza kumchapa kwa fimbo na kama haitoshi alichukua panga
lakini mwanae mwingine Hamis Abdala miaka (8) akamzuia ndipo alipochukua kisu
na kumkata kichwani mara mbili,” alisema Shana.
Alisema kuwa
wananchi baada ya kupata taarifa walifika na kuingilia kati ili kumwokoa mtoto
huyo na wao ndipo walipomshambulia na kumjeruhi kichwani na kisogoni kisha
walimfikisha polisi.
“Mtuhumiwa
alipatiwa matibabu na kwa sasa bado yuko mahabusu na amekemea tabia ya vitendo
vya ukatili kwa wanawake na watoto ambapo upelelezi umekamilika na mtuhumiwa
alitarajiwa kufikishwa mahakamani jana,” alisema Shana.
Awali
akizungumzia juu ya tukio hilo mwenyekiti wa mtaa wa Bamba Amri Mavalla alisema
kuwa wakati mtuhumiwa huyo akimwadhibu mama mzazi wa mtoto huyo ambaye ni
mjamzito alipoteza fahamu kwa hofu kwa mwanae.
Mavalla
alisema kuwa aliletewa taarifa majira ya saa 6 ofisini kwake na ndipo
alipokwenda kupata taarifa juu ya tukio hilo ambapo mama mzazi wa mtoto huyo
alishindwa kuchukua yoyote wakati baba yake akimwadhibu kutokana na hali yake.
Alisema kuwa
baada ya tukio hilo wasamaria wema walimpa huduma ya kwanza mama huyo wakati
huo wakimkimbiza mtoto huyo kituo cha afya cha Kongowe kwa ajili ya matibabu
ambapo anaendelea vizuri.
“Mtoto
huyo alichukua mayai hayo akiwa anacheza na wenzake lakini yeye peke yake ndiye
aliyeadhibiwa na wenzake hawakuchukuliwa hatua yoyote na ameshonwa nyuzi 12
utosini na nyuzi nane karibu na sikio,”
alisema Mavalla.
Aidha
alisema kuwa mtuhumiwa huyo alibadilisha nguo akiwa na lengo la kutaka kukimbia
na alipoulizwa kampiga mwanae na nini alisema kamchapa tu na fimbo.
Mwisho.
Subscribe to:
Posts (Atom)