Monday, October 28, 2013

KIPOZI NA ELIMU

Na John Gagarini, Bagamoyo
WILAYA ya Bagamoyo mkoa Pwani imeweka mkakati wa kuhakikisha wanafunzi wote waliopata nafasi ya kwenda sekondari wilayani humo wanakwenda shule na kuondokana na dhana kuwa mkoa huo hauna mwamko wa elimu.
Hayo yalisemwa na mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Bw Ahmed Kipozi wakati wa mahafali ya 22 ya shule ya sekondari ya Lugoba na kusema kuwa tayari wameshakutana na wadau mbalimbali yakiwemo mashirika yasiyo ya kiserikali na wazazi ili kufanikisha suala hilo.
Kipozi alibainisha kuwa moja ya mkakati huo ni ule wa ujenzi wa hosteli kwenye baadhi ya maeneo ili kuwapunguzia umbali wanafunzi ambapo moja ya changamoto imeonyesha kuwa umbali nao umekuwa chanzo cha wanafunzi kutopenda shule.
“Kwa sasa tumeunganisha nguvu ya pamoja na wadau wa elimu ndani ya wilaya ili kuhakikisha malengo ya watoto kwenda shule kwa kiwango kikubwa yanafikiwa ambapo washikadau wametuunga mkono na tunaamini mabadiliko yanaonekana kama leo unavyoona watoto wengi wamemaliza elimu yao ya sekondari,” alisema Bw Kipozi.
Awali mwalimu mkuu wa wa shule hiyo Bw Alhaj Abdalla Sakasa alisema kuwa anaomba wadau wa elimu kujitokeza kuwasaidia kupata fedha kwa ajili ya kugharamia vifaa vya maabara na kemikali kwa ajili ya wanafunzi wa kidato cha nne na cha sita kwani gharama ni kubwa sana.
Alhaj Sakasa alisema kuwa shule yake ina wanafunzi wengi wa masomo ya Sayansi hivyo kufanya maandalizi ya na kuendesha mitihani hiyo ya kitaifa kutumia gharama kubwa ambazo kwa sasa hawana.
“Gharama kwa wanafunzi wa kidato cha nne ni shilingi milioni 5.8 na kidato cha sita ni shilingi milioni 7 ambazo hadi sasa hatuna licha ya kuwa serikali inatoa ruzuku lakini ni kidogo sana  ukilinganisha na gharama halisi,” alisema Alhaj Sakasa.
Aidha alisema kuwa wazazi wengi hawana uwezo wa kulipia chakula kama ilivyoamuriwa ambapo kila mwanafunzi anapaswa kuchangia kiasi cha shilingi 100,000 kwa muhula ambazo wazazi wanshindwa kulipa.
Aliongeza kuwa wanampongeza mlezi wa shule hiyo Bw Subbash Patel kwa kuisaidia shule na watumishi wa shule ambapo aliwasaidia vifaa vya ujenzi na baadhi wamefanikiwa kujenga nyumba zao za kuishi, Katika mahafali hayo jumla ya wanafunzi 212 walipewa vyeti vya kuhitimu kidato cha nne ambapo shule hiyo ina wanafunzi 1,228 na walimu 57.

Mwisho.